Wednesday, July 29, 2015

MIAKA SITA YA TASHOKA (2009-2015)

MIAKA SITA YA TASHOKA (2009-2015)

********************************************************************************
Kila uongozi wa taasisi au shirikisho fulani huwa na malengo yanayo ambatana na majukumu yanayopaswa kutekelezwa kwa mujibu wa kanuni na taratibu zilizopo. Shirikisho la karate la staili ya Shotokan Tanzania (TASHOKA) chini ya uongozi wa mwenyekiti wake (Sensei Phillip Chikoko) limekuwa na mafanikio ya kuridhisha katika kuendeleza sanaa hii ya mapigano ukilinganisha na miaka ya nyuma. Lakini kama tujuavyo kuwa hakuna uongozi usio na changamoto. Hata hivyo huwa inasikitisha sana kunapotokea changamoto ambazo si za lazima na ambazo kwa mara kadhaa zimekuwa zikisababishwa na wadau wenyewe.
Ikumbukwe kuwa kazi inayofanywa na uongozi wa TASHOKA ni ya kujitolea. Hakuna mshahara/posho yoyote kutoka mahala popote. Hivyo uamuzi wa kuwa kiongozi wa TASHOKA unapaswa kusukumwa na uzalendo pamoja na nia njema na ya dhati ya kuiendeleza sanaa hii ya mapigano. Ni kazi ngumu inayohitaji moyo na umoja usiotetereka. Siyo kazi ya kukimbiliwa na mtu au watu fulani kwa kuwa hakuna maslahi zaidi ya kukumbukwa na historia ya karate hapa Tanzania. Lakini pia watu wasio na nia njema huweza kuutumia mwanya wa kutaka uongozi ili kujipatia fedha kwa kutumia njia za kilaghai au zisizo sahihi mfano kugushi vyeti, mihuri, kutoa madaraja ya uongo, n.k.

MAPUNGUFU YALIYOKUWEPO NA KUFANIKIWA KUTATUA
******************************************************************************
a) Palikuwa na klabu chache zilizosajiliwa ambapo uongozi huu ulijaribu kuhamasisha vilabu vingi vijisajili.
b) Hapakuwa na waalimu waliofahamu sheria za mashindano hapa nchini kiasi kwamba Tanzania ililazimika kuomba waamuzi toka Kenya kuchezesha mashindano. Tatizo hili lilitatuliwa na uongozi huu kwa msaada wa Sensei Kaneto toka Japan kupitia CCP Moshi na hatimae hapo baadae TASHOKA iliendesha semina kadhaa za mara kwa mara bure za mafunzo haya chini ya Sensei Chikoko ili kuwezesha wengi kuhudhuria na kufaidika. TASHOKA kwa mpango huu ikafanikiwa kuwa na waamuzi ambao waliweza kuendesha na kusimamia mashindano yao bila kutegemea waamuzi toka nje. Sambamba na hili, TASHOKA ilifanikiwa kubuni taratibu za kuelimisha waamuzi na hata kutengeneza vyeti kwa ajili ya hilo (copy BMT).
c) Wanafunzi wa Karate walitegemea vyeti vya klabu vya madaraja hata ya mkanda mweusi toka kwa waalimu wao ambavyo havikuweza kutambulika nje ya mipaka ya Tanzania. TASHOKA hii ilibuni vyeti vyake vyenye hadhi ya Kitaifa ili kukabiliana na tatizo hilo (copy BMT).
d) TASHOKA hii ilibuni taratibu za kuwapatia vyeti vyenye hadhi ya Kitaifa kwa kuwatahini wanakarate waliokusudia kuwa waalimu na ilifanikiwa kufanya hivyo kwa baadhi ya wakufunzi. Sambamba na hili iliendesha semina nyingi za bure za mafunzo haya chini ya Sensei Chikoko ili kuwezesha wengi kuhudhuria na kufaidika.
e) Uongozi huu chini ya Sensei Chikoko ndiyo ulioshiriki katika kuasisi Shirikisho la Karate Tanzania TKF(TANZANIA KARATE FEDERATION).
f) Ulijiwekea taratibu za kuandaa mashindano mara mbili kila mwaka.
g) Mbali na sababu zilizoainishwa hapo juu, TASHOKA ilibuni taratibu hizi ili kujipatia fedha za kuendesha shughuli zake ikiwemo ratiba za matukio kama vile mashindano nk.
h) TASHOKA ilikubali kutambua vikundi vya matawi ya mashirikisho ya kimataifa na kubariki shughuli zao kwa vile vilabu mwanachama wake tu.

CHANGAMOTO ZILIZOJITOKEZA NA ZILIZOPO
***************************************************************
a) Baadhi ya waalimu hawakuwa tayari kuingia darasani na kujifunza sheria za mashindano pamoja na kwamba hawakuwa wanazijua na kwa hiyo walihujumu mpango huo na mingine yote iliyofanana na utaratibu huo. Pamoja na TASHOKA kuendelea na mipango hii, lakini haikuweza kufanikisha lengo lililokusudiwa ikiwemo kujipatia mapato.
b) Baadhi ya waalimu viongozi walihujumu vyeti vya TASHOKA kwa kuvitoa kinyume cha sheria kwa manufaa binafsi. Hali hii iliilisababisha waalimu viongozi wa namna hii kuhujumu mpango huu pia kwa kuhamasisha vilabu mbalimbali ndani na nje ya mkoa wa Dar es salaam kutoshiriki katika mpango huu. Hili nalo limevuruga mpango wa mapato wa TASHOKA.
c) Pamoja na uongozi huu kusaidia baadhi ya vilabu kupata usajili toka kwa ofisi ya msajili wa serikali wa vyama na vilabu vya michezo, vilabu vingi vimekwepa kuwa mwanachama wa TASHOKA kutokana na mashinikizo ya tofauti za kisiasa. Kutokana na vilabu hivyo kukosa sifa ya uanachama wa TASHOKA, sababu hiyo imekuwa kikwazo kwao kushiriki mashindano yanayoandaliwa na TASHOKA na hivyo kuyazorotesha.
i) Pamoja na uongozi wa TASHOKA kukubali na kutambua vikundi vya matawi ya mashirikisho ya kimataifa na kubariki shughuli zao kwa vile vilabu mwanachama wake, baadhi ya vikundi vya namna hii viligeuka na kutaka kusajili vyama/ chama pinzani kwa TASHOKA, hata hivyo pamoja na vyama vya namna hii kuihujumu TASHOKA kwa azma ya kufanikisha ukuaji wake, malengo hayo yalishindikana kutokana na taratibu za ofisi ya msajili wa serikali wa vyama na vilabu vya michezo kutosajili chama zaidi ya kimoja kwa staili moja.
d) Pia maswala ya karate kuhusishwa na vikundi vya ugaidi yametumika kama silaha kwa waalimu, vilabu na vikundi vyenye itikadi fulani ili kupinga mikakati ya uongozi huu.
UONGOZI (TASHOKA)

No comments:

Post a Comment